Header Ads Widget

Responsive Advertisement

MADA: UHALISIA WA TENDI ZA KISWAHILI KATIKA JAMII YA KISASA; MFANO KUTOKA UTENZI WA FUMO LIYONGO






UHALISIA WA TENDI ZA KISWAHILI KATIKA JAMII YA SASA ;MFANO KUTOKA UTENZI WA FUMO LIYONGO.

Dutwa Dutwa

Iksiri

Makala hii imejikita katika kuangalia uhalisia wa tendi za kiswahili katika jamii ya sasa ya maendeleo ya sayansi na teknolojia. Dhana ya tendi imekua ikihusishwa sana  na historia (yaani ekiolojia) ikihusisha mambo ya kale yaani visa na matukio ambayo yalitendeka zamani. Dhana hii ya kuhusisha tendi na mambo ya kale ndiyo inapelekea dhana hii kuonekana kuwa ni mambo ya kale tu na kukosa uhalisia katika jamii ya sasa. Kwahiyo makala hii imejikita katika kuangalia namna tendi za Kiswahili, mfano kutoka katika utendi wa Fumo Lyongo jinsi ambavyo fani(lugha) na  maudhui hayo yanavyosawiri uhalisia katika jamii ya sasa. Hivyo itaonesha kama tendi za kiswahili zinasawiri maisha halisi ya jamii ya sasa au la.

1.0 Utangulizi

Tendi za Kiswahili zinahusishwa na historia za jamii mbalimbali kwa kuangazia visa na matukio yaliyopata kutokea au yanaaminika na wanajamii kuwa yalipata kutokea katika jamii husika. Jambo la kujiuliza ni kuwa je tendi za Kiswahili katika maudhui yake zinabeba uhalisia wa jamii ya sasa au ni dhana ambayo inabaki kuwa ni historia tu ambayo inaaminika kuwa ilitokea na siyo dhana inayoweza kurejelea jamii za kisasa ambazo zimeendelea zaidi ya zile jamii za kale. Dhana hii ya ukale au historia katika tendi zimeshadidiwa na wataalamu kama vile Chadwick’s (1932)  ambaye alichunguza masimulizi ya kijadi, na kuona kuwa mashujaa wanaakisi historia. Mtaaalamu mwingine anayeonyesha dhana ya historia katika tendi ni  Vansina (1965) ambaye katika kuthibitisha historia katika utendi,alionyesha vitu viwili yaani ukweli wa kihistoria na uhakika wa kihistoria. Anaeleza kuwa ukweli wa kihistoria ni sharti uweze kukubaliwa na kuaminiwa na watu wengi katika jamii. Mashujaa wakuu huakisi moja kwa moja historia.

huweza kueleza ukweli wa kihistoria na si hakika ya kihistoria. Pia Mulokozi (2002) anashadadia uwepo wa historia katika tendi wa kusema kuwa shujaa hawezi kuwa nje ya historia. Vitu hivi vinakamilishana, ukijumuisha na ubunifu wa kisanaa. Shujaa huakisi mfano halisi katika historia na vipindi vinavyozunguka matukio ya kihistoria. Mara nyingi katika tendi, matukio na mashujaa

Hivyo maelezo ya wataalamu hao yanathibitisha kuwa tendi hubeba historia za jamii kuhusu visa na matukio yaliyopita . Hivyo kuacha swali je zinaendana na jamii ya sasa kiuhalisia au zinabaki tu kuwa kama amali ya ukumbusho kwa kizazi cha sasa?.











1.1 Mawanda ya utafiti wa makala hii

Makala hii, imejikita katika kuangalia uhalisia wa tendi za Kiswahili kwa kuangalia uhalisia huo katika utendi wa Fumo Lyongo, uliotungwa na Muhammad Abubakar Kijumwa (1913). Kuna tendi mbalimbali za Kiswahili zinazoweza kuangazia mada ya utafiti uliofanywa na mwandishi wa makala hii, lakini ulichaguliwa utendi huu kuziwakilisha tendi nyingine zinazoweza kuangaziwa ili kuangalia uhalisia wa tendi hizo katika jamii ya sasa ya watanzania na Waafrika kwa ujumla. Mwandishi ameweza kueleza dhana ya jamii ya sasa kwa kurejelea jamii ya karne ya na 20 na kuendelea ambayo imepiga hatua zaidi katika maendeleo ya sayansi na teknolojia.

1.2 Kiunzi cha nadharia

Makala hii imeabiri mambo mbalimbali kwa kuzingatia nadharia ya uhalisia. Ntarangwi(2004) anasema kuwa nadharia hii katika upana wake, humaanisha uwakilishi wa uhalisi wa mambo katika fasihi. Mhalisia huamini katika matokeo ya mambo na ukweli anaouzingatia ni ule unaoweza kuonekana na kuthibitishwa kwa tajriba.

   2.0 Dhana ya Tendi

Kwa mujibu wa Bowra (1952) tendi ni masimulizi marefu ambayo yanahusu matukio yenye uzito na muhimu kwenye jamii.Mara nyingi tendi zinahusu masuala ya vita.



     Mulokozi (2002) Utendi ni ushairi wa matendo na ni utungo mrefu wenye kuzungumzia                       matukio ya kishujaa yenye uzito wa kijamii, kitaifa. Historia, visasili na Visakale.

TUKI (2013) tendi pia utenzi, hasa wenye kuhusu matukio ya ushujaa. Hivyo fasili hii inasisitiza kuwa tendi huzungumzia zaidi kuhusu matukio yaliyotendwa na mashujaa mbalimbali waliopata kutokea katika jamii.

      2.1 Kuhusu mtunzi

Mulokozi (1999) anaeleza kuwa Muhamadi Abubakar Kijumwa alikuwa mwenyeji wa Lamu nchini Kenya. Alikuwa msanii mashuhuri ambaye, mbali na kutunga mashairi na tendi, vilevile alikuwa mjomi ( mchongaji wa milango yenye nakshi), msanii-msanifu, msawidi  na mnukuzi wa miswada ya zamani. Habari za maisha yake hazijulikani vizuri. Alianza kujitokeza katika utunzi kwenye miaka ya 1890, alipoanza kuwasaidia watafiti wa kizungu waliotaka kufahamu habari za waswahili. Baadhi ya watafiti mashuhuri aliowasaidia ni Alice Werner (miaka ya 1930) na Ernst Dammann (miaka ya 1900-1940). Alifariki mwanzoni mwa miaka ya 1940 ( hatukufanikiwa kupata tarehe halisi ya kifo chake). Mtoto wake wa kiume aitwaye Elewa aliishi Lamu (hatuna hakika kama bado yu hai), na mjukuu wake, Esha Elewa anaishi Saudi Arabia ambako ameolewa. Mbali na utendi wa Fumo Liyongo, kijumwa alitunga mashairi mengine kadha ambayo si mashuhuri, ukiwemo Utendi wa Helewa( Siraji).



      2.2 Muhtasari wa kisa cha Fumo Liyongo

Kisa cha Liyongo kinahusu mgogoro kati ya Fumo Liyongo na kaka yake, mfalme wa Pate, ambaye katika utendi huu hatajwi jina lake, bali katika mapokezi mengine anaitwa Daudi Mringwari. Hadithi inaanza Liyongo akiwa ni kijana amekwisha balehe, mwenye kusifiwa nchini kote kwa nguvu na ushujaa wake. Anaishi nyumbani kwake Ungwana wa Mashaha ( eneo la Shaka, jimbo la Ozi). Ujumbe wa Wagalla unafika Pate kumtembelea Sultani Daudi. Sultani anamsifia Liyongo kwa Wagalla, lakini wao hawaamini maneno yake. Anampelekea barua Liyongo ya kumwita na Liyongo anaitikia wito huo kwa kufika barazani kwa Sultani. Wagalla wanakiri kweli Liyongo ni mtu mwenye nguvu. Wanamwomba Sultani awaruhusu wachukue mbegu yake, sultani anakubali na Liyongo anaozwa mke wa kigalla na kupata mtoto wa kiume . Mfalme anaingiwa na hofu ya kupinduliwa na Liyongo, anaanza  njama za kumuua kisha Liyongo anagundua njama hizo na hatimaye anakimbilia mwituni miongoni mwa Wasanye na Wadahalo na kufanya naye urafiki.Liyongo anakamatwa na kufungwa gerezani lakini anafanikiwa kutoroka. Baada ya jaribio hilo kushindwa mfalme anamtumia mwana wa Liyongo kumpeleleza na kujua siri ya namna ya kumuua Fumo Liyongo. Anafanikiwa kuijua siri na hatimaye kumuua baba yake kwa kumchoma sindano ya shaba kitovuni akiwa usingizini. Mwishoni mfalme anapata habari za kifo cha Liyongo, hivyo anafurahi sana lakini anamsaliti mtoto wa Liyongo kwa kumnyang`anya vitu alivyompa na hatimaye anaenda porini kwa Wagalla na kufia huko.





























Katika kutazama uhalisia wa tendi za kiswahili katika jamii za sasa. Makala hii itajikita katika kutazama lugha inayotumiwa na mtunzi wa utendi huu, pamoja na  maudhui yanayobebwa na  utendi huu  Utenzi wa Fumo Liyongo, uliotungwa na Muhammadi Abubakar Kijumwa (1913) . Tunaangazia vipengele vifuatavyo ili kubaini uhalisia  wa utendi huu katika jamii ya sasa:

3.0 Lugha iliyotumiwa na mtunzi

Kwa mujibu wa Wamitila (2003), lugha hutumiwa kuelezea mfumo wa sauti za nasibu zinazotumika na watu wa jamii fulani wenye utamaduni unaofanana, kuwasiliana. Lugha ina nafasi kubwa sana katika fasihi kwa kuwa fasihi yenyewe ni sanaa ya lugha. Lugha ndiyo nyenzo inayotofautisha fasihi na sanaa nyingine kama uchoraji, ufinyanzi, udarizi n.k. Lugha ni uchunguzi wowote wa kazi hizo hauna budi kuangalia suala la  kazi ya kifasihi, huyawasilisha maudhui yake. Dhamira yake na maana yake kwa kutegemea lugha. Baadhi ya wahakiki wa fasihi huitumia lugha kwa namna maalumu.

Kipengele cha lugha ni muhimu sana katika uwasilishaji wa kazi ya sanaa, kwani lugha ndiyo silaha ya mtunzi wa kazi ya fasihi ikiwemo utendi. Katika utendi huo, lugha iliyotumika ni ile yenye lahaja ya kiamu kwa kiasi kikubwa. Lahaja hii inakosa wazungumzaji wengi katika jamii ya sasa ya watanzania na hivyo kupelekea ugumu wa kuweza kuusoma utenzi huu na kuuelewa papo hapo bila ya kutatizwa na suala  la lugha iliyotumiwa na mwandishi (Muhammad Abubakar Kijumwa). Hali hii inapelekea watu wengi kushindwa kuusoma utenzi huu na kuuelewa bila ya kurejelea maana za maneno hayo ili waweze kupata maana kamili iliyokusudiwa na mwandishi na hivyo kusababisha ugumu wa kuusoma na kuelewa ujumbe uliomo ukilinganisha fani nyingine za fasihi kama vile riwaya, tamthiliya. Katika kuthibitisha suala la matumizi ya lugha isiyoeleweka na idadi kubwa ya watanzania wa sasa hebu tutazame baadhi ya beti zinazotoka katika utenzi huu

                                                             15.

Mato kikodoleya

Ghafula utazimiya

Kufaa kutakurubiya

Khufa kuingiya



                                                          16.

Wagala wakipulika

Kwa dhihaka wakateka

Wakanena “Twamtaka

Na sisi kumwangaliya.



                                                          161.

Kamfanyiza zakula

Za ndiani ili kula

Uwe mwana wa Kigala

Katoka kashika ndiya



                                                          162.

Naye chanenda ndiani

Una khaufu mouoni

“nifanye shauri gani



                                                            163.

Yakumu ya matatizo

“ iye mimi kumpata

Kutokufa ni matata

Taniumwa Mara moya..”



Beti hizo ni mfano tu wa beti zote zilizotumiwa na mtunzi katika kufikisha ujumbe wake kwa hadhira. Lakini tukiangazia uhalisia wa lugha iliyotumika katika beti hizo, tunatambua kuwa ni lugha ya Kiswahili kilichotumika ni kile kilichosheheni matumizi makubwa ya lahaja ya Kiamu. Hivyo tukitazama uhalisia wa lugha hiyo na Kiswahili sanifu ambacho ndiyo kinazungumzwa na watu wengi katika jamii ya sasa ya watanzania utaona kuwa watu wengi wa hii leo wanashindwa kutambua maana za maneno mengi yaliyotumiwa na mtunzi katika kufikisha ujumbe wake kwa jamii husika katika kipindi hicho. Hivyo matumizi ya lahaja ya kiamu imepelekea baadhi ya wasomaji kuona kuwa utendi ni kazi ya fasihi inayotumia lugha ngumu katika kuwasilisha ujumbe wake kwa hadhira. Lugha ya Kiswahili sanifu ni ile iliyosanifishwa kutoka katika lahaja ya kiunguja. Katika jamii ya sasa ya Watanzania Kiswahili na wanaosoma tendi, Kiswahili chenye lahaja ya kiamu hakina wigo mkubwa kimatumizi na hivyo hali hii inapelekea ugumu wa kuelewa kile kinachowasilishwa na mtunzi wa utendi kwa urahisi.







 4.0 Maudhui

Kwa mujibu wa Wamitila (2003), maudhui ni jumla ya mambo yote yanayozungumziwa katika  kazi ya fasihi. Maudhui hutumiwa kwa upana kujumlisha dhamira, falsafa, itikadi na msimamo. Hivyo maudhui ni jumla ya mambo yote anayotoa fanani au msanii wa kazi ya fasihi kupitia mbinu mbalimbali alizozitumia ili kufikisha ujumbe kwa hadhira aliyoikusudia.Maudhui yaliyomo katika tendi za Kiswahili hususani Fumo Liyongo ni pamoja na:

4.1 Ushujaa katika utendi  

Kwa mujibu wa Wamitila (2003), shujaa ni mhusika mkuu katika kazi ya kifasihi ambaye anaweza kuwa wa kike au wa kiume. Kimsingi neno hili haliashirii wema tu, mhusika mkuu anaweza kuwa mbaya.

TUKI (2013), shujaa ni mtu mwenye moyo thabiti anayeweza kukabili mambo, hata kama ni ya hatari.

Kama ilivyo maana ya utendi kuwa ni masimulizi marefu ya kinudhumu yenye kuelezea matendo ya kishujaa. Hivyo tendi hutawaliwa na matendo yanayotendwa na shujaa husika katika kuleta maudhui yenye ujumbe fulani kwa jamii. Hapa tutaangazia sifa mbalimbali za shujaa wa Kiswahili, hususani Fumo Liyongo ili kuona kama sifa za shujaa huyu zinasawiri au kwenda sambamba na sifa za mashujaa wa kisasa na kama  tofauti zozote baina yao. Sifa za Shujaa wa tendi za Kiswahili. Kwa mijibu wa Mulokozi (1999 & 2002) ni

4.1.1 Anatoka tabaka lolote

Shujaa wa Kiswahili katika tendi huweza kutoka tabaka lolote na hatimaye kuweza kutenda matendo ya kishujaa ambayo yanadhihirisha ushujaa wake. Katika utenzi wa Fumo Liyongo, shujaa Lyongo, hatuelezwi wazi na mwandishi kama anatoka katika tabaka lipi lakini inasemekana kuwa alitoka tabaka la juu, kwani adui yake mfalme Daudi Mringwari anasemekana kuwa alikua ndugu yake wa damu. Ambapo Liyongo alikimbia mji wa Pate ulikokuwa ukitawaliwa na nduguye kwasababu ya visa vya nduguye.Pia hata katika utenzi wa Rasil Ighul, shujaa mkuu Mtume Muhamamad (S.A.W) anatoka katika tabaka la chini lakini anaibuka kuwa shujaa katika kuongoza vita dhidi ya wasiokuwa waumini wa uislamu. Sifa hii ya shujaa inasawirika hadi katika jamii ya sasa, kwani mashujaa wake wametoka katika matabaka tofauti tofauti. Mfano shujaa wa taifa la Tanganyika Julius k Nyerere alitoka katika tabaka la juu kiuchumi kwani baba yake alikuwa ni chifu.

4.1.2 Shujaa huwa jasiri

Kwa mujibu wa TUKI (2013), Ujasiri ni hali ya kukabili jambo bila ya hofu. Hivyo ujasiri huonyesha kuwa shujaa ni mtu anayejiamni katika kukabiliana na changamoto mbalimbali anazokutana nazo.

Katika utendi huu shujaa Liyongo ni mtu jasiri anayeweza kupambana na kundi la watu na kuwashinda, anafanikiwa kutoroka hata jela kwa kutumia tupa.Ujasiri wake ndiyo unaomchochea kutenda matendo ya kishujaa, matendo yaliyomwogopesha Sultwani. Katika kuonyesha dhana ya ujasiri kwa shujaa Liyongo, mtunzi anabainisha katika beti zifuatazo

                                                      7.

Kimo kawa mtukufu

Mpana sana mrefu

Majimboni yu maarufu

Watu huya kwangaliya

                                          



                                                          12.

Mfalme kawambiya

Wagala kiwasifiya

Huwegemea watu miya

Wasiweze kukimbiya



                                                          13.

mwanamume swahihi

 Ni Kama simba unazihi

Usiku na asubuhi

 Kutembeya ni mamoya

Sifa hii ya ujasiri inadhihirika hata katika mashujaa wa jamii ya sasa kwani huwezi kutenda matendo ya kishujaa katika jamii bila ya kuwa na ujasiri unaokuchochea kutenda matendo hayo. Mfano shujaa wa taifa la Afrika kusini , Nelson Mandela alikuwa na ujasiri wa kuwapinga makaburu walioogopwa na jamii ya watu wengi lakini yeye alijitokeza hadharani katika kuwapinga. Kitendo hiko kinachoonyesha ujasiri wa hali ya juu aliokuwa nao Nelson Mandela.

4.1.3 Uogofu (aogopwe), shujaa wa Kiswahili anatakiwa aogopwe kutokana na matendo ya kutisha au yasiyo ya kawaida yanayotendwa na shujaa huyo. Katika utenzi wa Fumo Liyongo, shujaa Liyongo anaonekana kuogopwa kutokana na matendo yake ya kishujaa anayoweza kuyatenda kutokana na nguvu za ajabu alizokuwa nazo. Suala hili linathibitika kupitia beti zifuatazo

                                  



                                                   12.

Mfalme kawambiya

Wagala kinasifiya

Huwegemea watu miya

Wasiweze kukimbiya.



                                                         14.

Ghafula kikutokeya

Mkoyo hukupoteya

Tapo ukikumiliya

Ukatapa na kuliya.



                                   

                                                             15.

Mato kikodololeya

Ghafula utazimiya

Kufaa kutakurubiya

Kwa khaufu kuingiya





                                                          16.

Wagala wakipulika

Kwa dhihaka wakateka

Wakanena “ twamtaka

Na sisi kumwangaliya”

Mfano wa beti hizi ni baadhi tu ya zile zinazomwonyesha shujaa Liyongo ambaye anamiminiwa sifa kedekede na mfalme wa Pate, kwa matendo yake na haiba yake. Haiba yake inaonyeshwa kama mtu anayetisha ukikutana naye uso kwa uso kwani akikukodolea macho yake unaweza kuzimia. Katika jamii ya sasa shujaa si lazima atishe kwani mashujaa hutumia zaidi akili kuliko nguvu kama ilivyokuwa katika jamii zamani. Shujaa wa kisasa hutumia maneno katika kuhamasisha na kuleta mapinduzi au maendeleo chanya kwa jamii yake inayomzunguka. Mfano, Rais Magufuli ni shujaa katika jamii ya watanzania wa leo lakini siyo mtu anayetisha kimuonekano, lakini hutumua maneno tu katika kutoa maagizo na maelekezo kwa viongozi wengine na hivyo kupelekea maendeleo katika nchi yetu.



4.1.4 Shujaa huwa rijali

Kama ilivvyo kawaida katika tendi za Kiafrika, nguvu za kimwili za shujaa wa utendi wa Kiswahili huambatana na urijali ambapo shujaa huwa na uwezo wa kufanya mapenzi na mwanamke/ wanawake kwa muda mrefu bila ya kuchoka. Katika utendi huu Wagalla wanavutiwa na umbo la Liyongo, wanataka wapate “mbegu yake na wanaipata “ . Suala hili linaweza kuonekana katika beti zifuatazo

                                                 

                                                           6.

Liyongo kitamkali

Akabalighi rijali

Akawa mtu wa kweli

Na haiba kaongeya

                                                          

                                                      40.

                                                         Wagala wakabaini

Kumwambia sulutwani

Twamtaka kwa thamani

Kijana kutuweleya



                                                         41.   

Twaitaka mbeu yake

Nasi kwetu tuipeke

Kwa furaha tumuweke

Apate kutuzaliya.

Sifa hii ya urijali kwa shujaa katika jamii ya sasa haina mashiko kwani shujaa hupaswa kufanya mambo yale chanya na muhimu kwa jamii yake na siyo kufanya mapenzi, pia katika jamii ya sasa magonjwa ya zinaa ni mengi ukiwemo Upungufu wa Kinga Mwilini (UKIMWI).

 4.1.5 mashujaa wake  wakuu ni wanaume tu. Pia katika tendi karibia zote alizozisoma mwandishi, Ilibainika kuwa katika tendi za Kiswahili mashujaa wote ni wanaume hivyo kuleta dhana ya mfumo dume uliopo katika jamii kwa kuona kuwa wanaume tu ndo huweza kutenda matendo ya kishujaa. Mfano, shujaa Nyakiiru na Kanyamaishwa katika Utendi wa Nyakiiru Kibi, Mtume Muhammad katika utendi wa Rasil Ighul. Katika utenzi wa Fumo Liyongo, Tunaona kuwa shujaa mkuu ni Liyongo ambaye anaonekana kama mwanaume mwenye nguvu.

Suala hili ni tofauti au linakosa uhalisia katika jamii ya sasa ya watanzania na ulimwengu mzima  kwa ujumla kwani kuna dhana ya ufeministi ambayo imetawala katika jamii. Unasisitizwa usawa, pia katika jamii ya sasa kuna baadhi ya mashujaa wa kike. Kwa mfano Bibi titi Mohamed ambaye alishiriki katika kupigania uhuru wa Tanganyika kutoka kwa wakoloni akiwa sambamba na mwalimu Jukius k Nyerere.

Suala la kuwachukulia wanaume kuwa ndiyo mashujaa linaonyeshwa kupitia shujaa wa Utenzi wa Fumo Liyongo yaani Lyongo kupitia beti zifuatazo



                                            

                                                      13.

Ni mwanamume swahihi

Kama simba nazihi

Usiku na asubuhi

Kutembeya ni mamoya



                                                            15.

Mato kikodoleya

Ghafula utazimiya

Kufaa utakiruibiya

Kwa khaufa kuingiya



                                                      



                                                        16.

Wagala wakipulika

Kwa dhihaka wakateka

Wakanena “twamtaka

Na sisi kumwanagliya.”





4.2 Usaliti, katika tendi nyingi za Kiswahili hususani katika utendi huu, dhana ya usaliti imejitokeza wazi kwa mtoto wa shujaa Liyongo kumsaliti baba yake kutokana na uroho na uchu wa mali na madaraka. Usaliti huo ndiyo unapelekea anguko la shujaa hadi kusababisha kifo chake kwa kuwa tu alimpeleleza baba yake na kupata kutambua siri iliyo nyuma ya pazia kuhusu nguvu za baba yake baada ya kutumwa na Sultwani kumpeleza na kisha amuue baba yake. Hivyo anamuua baba yake kwa kutumia sindano ya shaba kwa kumchoma kitovun, alipokuwa usingizini. Mtunzi anathibitisha hili katika beti zifuatazo



                                                     143.

Nisikiya wangu baba

Liniuwalo ni baba

Ni msumari wa shaba

Kitovuni nikitiya



                                                           144.

Jamaasilaha ya

Haziniuwi swabiya

Ila nimezokwambiya

Ni ya kweli yote piya



                                               





                                                        145.

Kijana akisikiya

Shughuli lalimngiya

Kataka kusikiliya

Pate akanene haya.

Jambo hili la usaliti lipo hata katika jamii za sasa ambapo baadhi ya watu wamekua wakiwasaliti jamaa zao kwa tamaa mbalimbali zikiwemo za mali. Viongozi mbalimbali wa kisiasa wamekua wakisaliti wananchi wao kwa mataifa makubwa ya kibeberu. Kwa kukubali masharti magumu ya misaada na mikopo bila ya kuwashirikisha wananchi hao, hivyo huo ni usaliti kwani wananchi hao ndio wanawajibika kulipa mikopo hiyo kuipitia kodi zao.





4.3 Mgogoro kati ya tabaka tawala na tabaka tawaliwa likiongozwa na shujaa (Liyongo). Katuka utendi huu Liyongo anaonekana kuwa katika mgogoro na mfalme wa Pate, hali inayosababisha yeye kukimbia mji huo na kwenda kuishi porini. Ndipo mfalme anamtumia mwana wa damu wa Liyongo kwa kumlaghai kumpa sehemu nzuri ya kuishi akisaidiwa na wajakazi na kumuahidi kumuoza mwana wa mfalme akiifanikisha zoezi la kumuua baba yake. Mfame au sultan anafanya haya yote ili aweze kumuondoa Liyongo anayeishi katika tabaka tawaliwa. Anaonekana kutishia utawala wake kwani angeweza kumpindua muda wowote. Tuangazie beti zifuatazo



                                                 154.

                                                       Kamkirimu kijana

                                                       Kwa zitu kulla namna

                                                      Malalo mazuri sana

                                                      Winyi kumtumikiya



                                              156.

                                                        Kijana kafurahiya

                                                       tamaa zikamshika

                                                     “ na kuoa ni hakika

                                                       huwa watanitendeya



                                                     158.

                                                        Kisa kumi kutimiya

                                                        Sulutwani kamwambiya

                                                     “ hii sindano pokeya

                                                        haya kwake sikiliya..”

Suala la mgogoro kati ya tabaka tawala na lile tawaliwa bado lipo sana katika jamii ya sasa. Mashujaa kutoka tabaka tawaliwa wanaojaribu kupambana na tabaka tawala mara nyingi hupata madhila mengi ikiwamo kufa, kufungwa. Mfano Nelson Mandela wa Afrika kusini, aliyefungwa kwa miaka takribani 27 kwa kwa kupigania haki na maslahi ya watu weusi wa Afrika kusini waliokuwa wakikandamizwa na utawala wa kikatili wa mabeberu.



4.4 Tamaa au kugombania utawala na mali

Katika kuangalia dhana hii ya tamaa au uchu wa utawala katika utendi huu, mtunzi anamchora  Liyongo kama muhanga wa tamaa ya utawala ya Sultani  na mtoto wake. Ni mtu mwema anayeponzwa na wema na uwezo wake (Mulokozi 1999). Dhamira ya usaliti inawasiwiriwa tunamwona mwana wa Liyongo akirubuniwa hadi kumsaliti baba yake kwa tamaa ya mali na hadhi. Suala hili linaonyeshwa kupitia beti zifuatazo

                                               178.

                                                   Kayuwa hana fahamu

                                                   Kijana aliazimu

                                                   Kwa ile yakwe hamuhamu

                                                   Mke kwenda kuzengeya

                                             

                                             179.

                                                  Kamtiya kitovuni

                                                  Naye uleule kwa t`ani

                                                   Achamka hamuoni

                                                   Kiyana amekimbiya.

                                                    

                                          180.

                                                   Babake akishutuka

                                                   Chembe uta ukashika

                                                    Kwa haraka akatoka

                                                   Nde mui kayendeya

   Suala la hili la kugombania utawala na mali, linadhihirika wazi katika jamii ya sasa, kwani watu wamekua wakitumia hila na nguvu nyingi katika kupigania utawala, mfano viongozi au wanasiasa wengi kutoka bara la Afrika wamekuwa wakisababisha vita na migogoro mbalimbali kutokana na tamaa zao za kushika madaraka. Mathalani; Wanasiasa au viongozi wa Sudani Kusini Salva kiir na Riek Marshali wamekua wakisababisha vita na migogoro katika nchi hiyo kutokana na uchu wao wa madaraka, pia migogoro inayotokea katika nchi kama za Kongo D.R.C, Somalia chanzo kikubwa ni kupigania utawala.

                                                   

                                        

5.0 Hitimisho

Makala hii imegusia namna tendi za kiswahili zinavyosawirika katika jamii ya sasa kwa kuangalia uhalisia licha ya ukale wake. Pia katika sehemu hii ya hitimisho ninapendekeza kuwa lugha ya tendi mbalimbali za Kiswahili ni muhimu ikarahisishwa ili kuleta uhalisia wa kiswahili kama kinavyotumika katika jamii yetu ya kisasa. Pia zinaweza kuandikwa tendi juu ya matendo ya mashujaa wa kisasa waliopo katika jamii za kisasa zilizoendelea katika nyanja za sayansi na teknolojia, kuliko kubaki tu na tendi zinazoangazia matendo ya mashujaa yaliyotendwa kataka jamii za zamani.























    





                                                MAREJELEO

Bowra, C.M (1952). Heroic Poetry. London: Macmillan Publishers.

Mulokozi, M.M (1999). Tenzi Tatu Za Kale.Dar es Salaam: Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.

Mulokozi M.M (2002). The African Epic Controversy. Dar es Salaam: Mkuki na Nyota.

Ntarangwi, M (2004). Uhakiki wa kazi za Fasihi. Augustana College, Rock Island, IL 61201

Vansina, J (1965). Oral Tradition: A Study in Historical Methodology. Chicago: Aldine                             Publishing.

Wamitila, K.W (2003).   Kamusi ya Fasihi, Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus Publication Ltd.







              
JINA
NAMBA YA USAJILI
KOZI
SAHIHI
DUTWA DUTWA K
2016-04-02493
BAK


   



Post a Comment

0 Comments