Header Ads Widget

Responsive Advertisement

FASIHI YA WATOTO



Dhana ya fasihi imefasiliwa na wataalamu mbalimbali kama ifuatavyo mathalani, Massamba (1999) anasema kuwa fasihi ni sanaa inayotungwa au kubuniwa kwa lengo la kuifikishia ujumbe hadhira iliyokusudiwa kwa njia ya mdomo au maandishi.
Aidha, Wamitila (2010) anafasili fasihi kuwa ni sanaa inayotumia lugha kwa namna maalumu inayoathili na kupitisha ujumbe fulani unaolenga hadhira. Fasili hii ina mapungufu yake kwa kuwa haiweki bayana lugha hiyo ama ni ya mazungumzo au iko katika maandishi.
Kwa ujumla fasihi ni sanaa itumiayo lugha ama ya mazungumzo au ya maandishi ili kuweza kufikisha ujumbe kwa hadhira iliyokusudiwa. Hadhira hiyo inaweza kuwa ya watoto au watu wazima.
Pia, fasihi ya watoto imefasiliwa na wataaalamu mbalimbali kama ifuatavyo: Weche (2010) anafasili fasihi ya watoto kuwa ni kioo cha kumwongoza mtoto katika mambo mbalimbali yanayohusu maadili. Anaendela kueleza kuwa fasihi hiyo haina budi kupinga tabia zisizokubalika na kuzibainisha tabia hizo kwa watoto ili wazifahamu.
Wamitila (2008) anafasili fasihi ya watoto kuwa ni ile fasihi ambayo kimsingi hurejelea matini au kazi ambazo hadhira yake kubwa ni ya watoto.
NOUN (2010) wanaeleza kuwa fasihi ya watoto ni ile fasihi inayomlenga mtoto na siyo mtu mzima.Wanaendelea kueleza kuwa fasihi hii inaweza kuwa katika tanzu mbalimbali kama vile hadithi, ushairi, visakale na drama.
Vilevile, Wamitila (2010) anafasili fasihi ya watoto kuwa ni ile fasihi ambayo maudhui yake yamejengwa kwa ajili ya mtoto.
Fasili zote hufanya dhana ya fasihi ya watoto iwe telezi yaani itazamwe kwa namna mbalimbali kwa kuwa hazimuweki bayana mtoto anayezungumziwa ambapo kutokana na fasili hizo unaweza kujiuliza, Je mtoto anayemaanishwa ni yupi? Ili kufahamu nani ni mtoto hatuna budi kuangalia mitazamo ifuatayo:
Mtazamo wa kidini, katika mtazamo huu mtoto anachukuliwa ni mtu yeyote anayeamini kuwapo kwa Mungu kupitia dini. Waumini wote wa dini husika humuita Mungu kuwa ni baba, hivyo waumini wote huonekana watoto mblele ya Mungu na kuishi kwa kufuata mafundisho yake.
Mtoto katika mtazamo wa kikatiba, katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania humtambua mtoto kama mtu yeyote aliye chini ya miaka kumi na nane (18). Hivyo, yeyote aliye juu ya umri huo hachukuliwi kama mtoto bali ni mtu mzima.
Mtazamo wa kibaiolojia na ukuaji, pia mtazamo huu hutambua kuwa mtoto ni kiumbe chochote chenye viungo tete vinavyoendelea kukomaa na hadi kufikia kipindi cha kubalehe na kuingia utu uzima. Hivyo, mtazamo huu huona mtoto kama kiumbe chochote si lazima awe binadamu.
Mtazamo wa kihistoria, kijamii na kiutamaduni, kila jamii ina namna yake ya kumtambua mtoto ni nani kupitia masuala mbalimbali. Kwa mfano katika jamii ya Kitanzania hutenga mambo yanayofanywa na watoto na watu wazima. Kwa mfano jando na unyago hufanywa na watoto na vijana. Vilevile katika jamii mtoto ni mtu yeyote mwenye umri mdogo dhidi ya wakubwa au wazee. Hivyo, wazee huwaona vijana ni watoto bila kujali umri wao.
Hivyo basi, mtazamo wa kikatiba ndio mtazamo unaofaa zaidi katika kubainisha yupi hasa ni mtoto anayemaanishwa. Mtazamo huu hudai kwamba mtoto ni mtu mwenye umri chini ya miaka kumi na nane (18). Hivyo, kutokana na mtazamo huu tunaweza kusema kuwa fasihi ya watoto ni ile fasihi ambayo fani na maudhui yake humlenga mtu aliye chini ya miaka kumi na nane (18). Hata hivyo ieleweke kuwa kwa kiasi fulani huweza kuwahusu watu wazima yaani wale watu walio juu ya miaka kumi na nane.
Kwa kutumia kazi mbili za fasihi ya watoto ambazo ni riwaya ya Zindera iliyoandikwa na Erast G. Sabuni pamoja na tamthilia ya Kilio Chetu iliyoandikwa na Medical Aid Foundation, dhana ya fasihi ya watoto inaweza kufasiliwa kama ifuatavyo:
Wamitila (20100 anatoa sifa mbalimbali ambazo zinaweza kutumika kufasili dhana ya fasihi ya watoto kama ifuatavyo:
Fasihi ya watoto ni fasihi inayojikita zaidi kujadili masuala mbalimbali ya watoto na malezi yao kwa ujumla. Dhamira nyingi katika vitabu vya watoto na hulenga watoto kwa kiasi kikubwa. Kwa mfano katika riwaya ya Zindera masuala mbalimbali ya watoto walemavu yamejadiliwa. Kwa mfano kutengwa kwa watoto wenye ulemavu wa ngozi (albino). Kama ilivyokuwa kwa Zindera aliyekataliwa na baba yake. Kwa mfano Nzeta anasema;
“Masikini” ni kitoto cha kike lakini albino” (Uk. 4)
Pia, Mpanduji mume wa Sara anasema;
“Albino! Akamdondosha mtoto chini” (Uk)
Vilevile katika tamthilia ya Kilio Chetu  inajadili matatizo mbalimbali yanayowakabili watoto ikiwemo ukosefu wa elimu ya kijinsia inayosababisha watoto kupata maambukizi ya virusi vya UKIMWI pamoja na mimba za utotoni. Kwa mfano, Suzi anasema,
“Mie, kwanza sikujua mambo haya, mama na mjomba walijua juu ya mambo haya ya mapenzi”
Hivyo, watoto huwalaumu wazazi kwa kutowahadharisha mapema na kuwapatia elimu hiyo ya jinsia.
Mara nyingi fasihi ya watoto huwa na muundo sahili. Senkoro (2011) anaeleza muundo ni mtiririko wa visa na matukio katika kazi ya fasihi. Naye Wamitla (2010) anaeleza kuwa muundo wa fasihi ya watoto ni mwepesi unaomwezesha kupata ujumbe kwa njia rahisi. Muundo huu hutumika ili kuwafanya watoto waelewe kwa urahisimaudhui bila kuchanganyikiwa. Mfano katika riwaya ya Zindera imetumia muundo sahili (wa moja kwa moja) kwani matukio yamepangwa kuanzia ndoa ya Mpanduji na Sara, kuzaliwa kwa Zindera, matatizo aliyoyapatia na hatimaye kufanikiwa kuwa daktari. Hii imesaidia watoto kufuata mafunzo kwa njia rahisi. Vilevile, katika tamthilia ya Kilio Chetu muundo uliotumika ni wa moja kwa moja ambapo tunaona toka mwanzo kuingia kwa DUBWANA (UKIMWI) na jinsi watu walivyo kosa elimu ya ugonjwa huo na hatimaye kifo cha Joti na Suzi kutokea.
Wahusika wakuu katika fasihi ya watoto mara nyingi huwa ni watoto wenyewe. Njogu na Chimerah (2011) anaeleza kuwa wahusika ni sehemu ya kazi na viumbe wa sanaa inyobuniwa kutokana na mazingira ya msanii. Pia Wamitila (2010) anasema kuwa fasihi ya watoto lazima iwe na wahusika watoto wenyewe. Hiyo ni kwa ajili ya kuonesha uhalisia wa yale yanayozungumziwa, kujadiliwa na kutendwa na watoto wenyewe. Ketika tamthilia ya Kilio Chetu wahusika wakuu wote ni watoto wenyewe. Kwa mfano Joti, Suzi, Anna na Mwarami ambao huonekana toka mwanzo wa tamthilia hadi mwisho wakiwa wanalaumu madhara ya kukosa elimu ya jinsia. Kwa mfano Suzi anasema;
“….naapa kwa Mungu wangu, mimi na Joti tungepata bahati ya kuelimishwa tusingetumbu…tu…”
Pia, katika riwaya ya Zindera mhusika mkuu ni mtoto mwenyewe ambapo tunaona Zindera kuwa ndiye mhusika mkuu kuanzia mwanzo wa riwaya hadi mwisho (toka kuzaliwa kwake, malezi yake na hatimae mafanikio yake ya kuwa daktari).
Mara nyingi fasihi ya watoto hutumia yatima kama motifu. Ndalu na wenzake (2014) wanaeleza kuwa yatima ni mtoto aliyefiwa na mzazi mmoja au zaidi. Pia, Wamitila (2010) amnaeleza kuwa haiwezi kuchunguzwa bila ya kuchunguza nafasi ya mhusika au mtoto yatima au aliyetengwa na hivyo hulazimika kufanya juhudi za kujiokoa au kuishia kuokolewa. Motifu hii inatumika katika kazi nyingi za fasihi ya watoto kwa kukuza ujasiri na akili ya kuweza kujinasua kwenye mtego fulani. Hata hivyo ieleweke kuwa pale ambapo mtoto si yatima aghalabu huwa na upungufu au dosari fulani ya kimaumbile. Kwa mfano motifu hii imetumika katika riwaya ya Zindera pale ambapo Zindera alipotelekezwa porini. Licha ya changamoto alizopitia ikiwa ni pamoja na kufiwa na walezi wake lakini mwishowe anakuwa daktari. Kwa mfano mwandishi anaema:
“Katika hali ambayo haikutarajiwa, moto mkubwa ulizuka kijijini kwao. Moto huo uliteketeza kabisa myumba ya mwindaji Makale. Ni Pili pekee yake aliyenusurika kifo. Lakini Makale na mkewe wote walifariki dunia”
Pia, katika tamthilia ya Kilio Chetu motifu ya yatima imetumika kwani tunamuona mhusika Suzi ambaye alikuwa na mzazi mmoja tu wa kike.
Pia, fasihi ya watoto husheheni michoro, picha na vielelezo mbalimbali. Ngugi (2011) anaeleza kuwa kazi nyingi za watoto lazima ziwe na vielelezo, michoro pamoja na picha. Anaendelea kusema kuwa dhima yake kuu ni kufikisha ujumbe kwa njia iliyorahisi. Kwa mfano, kuna mchoro unaomuonesha Suzi akipigwa na mama yake baada ya kukutwa na vidonge vya majira kwenye nguo zake shule (Uk. 10).. Pia, katika riwaya ya Zindera kuna vielelezo mbalimbali vilivyotumika ili kufanya ujumbe uwafikie kwa urahisi kwa mfano kuna kielelezo kinachoonesha Sara akimficha mwanae Zindera baada ya kuhisi kuna mtu anamfuatilia kwa nia ya kumdhuru mwanae. (Uk. 15). Pia, vielelezo vingine viko katika ukurasa wa 2, 21, 28, 35, 45, 51, 58 na 65.
Fasihi ya watoto mara nyingi hutumia lugha rahisi inayoeleweka kwa urahis. Wamitila (2010) anafafanua kuwa lugha ni nyenzo kuu katika kazi yoyote ile ya fasihi. Anaendelea kueleza kuwa lugha nyepesi si lazima kwa watu wazima kwani uwezo wao ni mkubwa. hivyo Hivyo, fasihi ya watoto hutumia sentensi fupi na sentensi zisizochangamani. Lengo kuu la kutumia lugha nyepesi ili kufikisha ujumbe kwa njia iliyo rahisi. Kwa mfano katika tamthilia ya Kilio Chetu mwandishi anasema;
“Mwarami: Mshikaji Joti ee, umetuanika juani hivi
Joti: Kwani viti jamani?
Choggo: Eti vipi? We sio tulikubaliana kukutana pale  kijiweni?” (Uk. 18)
Vilevile, kitabu cha Zindera tunaona kuwa lugha iliyotumika miongoni mwa wahusika wa riwaya hii. Lugha hii imetumika ili maudhui yawafikie watoto kwa njia rahisi. Kwa mfano, mwandishi anasema;
“Ahsante baba, Zindera alisema” Zindera alisema sasa naweza kufanya upasuaji, nayafahamu maadhi mengi pamoja na tiba yake!
Kwa kuhitimisha, fasihi ya watoto ina dhima kubwa sana katika jamii si kwa watoto tu bali hata kwa watu wazima kwani licha ya watoto kupata elimu inayohusiana na namna gani ya kuishi na jamii inayowazunguka hususani watu wazima, lakini na fasihi hutoa njia mbalimbali zinazowasaidia wazazi kufahamu jinsi ya kuishi na kulea watoto.
MAREJELEO
Medical Aid Foundation (1995). Kilio Chetu. Dar es Salaam: TPH.
NOUN (2010). Children Literature. Lagos: National Open University of Nigeria.
Ngugi, P. (2010). Language and Literacy Education: The Stateof Chidrens in Kiswahili in Kenya. Berlin: Lambert Academic Publishing.
Njogu, k. na Chimerah, R. (2008) Ufundishaji wa Fasihi, Nadharia na Mbinu, Nairobi:Jomo Kenyatta Foundation. Ngugi, P. (2010). Language and Literacy Education: The Stateof Chidrens in Kiswahili in Kenya. Berlin: Lambert Academic Publishing
Mulokozi, M. M. (1996). Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili. Dar es Salaam: TUKI.
Ndalu na wenzake. (2014). Kamusi Teule ya Kiswahili. Dar es Salaam: EAEP.
Sabuni, E. G. (2008). Zindera. Dar es Salaam; Solution Publuishing.
Wamitila, K. W. (2010). Kichocheo cha Fasihi Simulizi na Andishi. Niarobi: Focus Books. Wamitila, K. W. (2008). Misingi ya Uchunguzi wa Fasihi. Nairobi: Vide Muwa Publishers.




Post a Comment

0 Comments