Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Hakuna lugha ya fasihi, jadili rai hili kwakutumia mawazo ya Wamitila 2008


Mjadala huu umegawanyika
katika sehemu kuu tatu, kwanza utangulizi ambapo tumefasili dhana mbalimbali zilizojitokeza katika swali hili, pili ni kiini cha swali ambapo tumeangalia lugha ya kifasihi kulingana na mawazo ya Wamitila. Katika sehemu ya hitimisho, tumehitimisha kwa kutumia mawazo yetu kulingana na namna swali linavyotaka.

Ufafanuzi wa Dhana Muhimu



Mulokozi (2017), Fasihi ni sanaa ya lugha yenye ubunifu unaojaribu kusawiri vipengele vya maisha, mahusiano, mazingira na hisia za watu katika muktadha fulani. Udhaifu wa fasili hii ni kuwa imesisitiza suala la ubunifu na kuacha vipengele vya lugha.

Naye M’ngaruthi (2015) anafasili fasihi kuwa ni kazi yoyote ya sanaa inayowasilishwa kupitia lugha ama iliyoandikwa au kutamkwa kwa njia ya ubunifu. Udhaifu wa fasili hii ni kuwa haijabainishwa imemlenga haswa nani.

Kwa ujumla, fasihi ni sanaa inayotumia lugha ili kufikisha ujumbe kwa jamii au hadhira iliyokusudiwa.

Wamitila (2016) anafasili lugha kuwa ni mfumo mzima wa sauti na maneno yanayotumiwa na watu kuwasiliana. Udhaifu wa fasili hii ni kwamba imeangalia suala la sauti kwa ujumla na kusahau kuwepo kwa sauti za nasibu.

Habwe na Karanja (2012) wanafasili lugha kuwa ni mfumo wa sauti za nasibu zinazotumiwa na watu wa jamii wenye utamaduni unaofanana ili kuwasiliana.

Kwa ujumla, lugha ni mpangilio au utaratibu wa sauti za nasibu zinazosemwa na watu wenye utamaduni mmoja ili kufikisha ujumbe kwa jamii.

Wamitila (2008) anaeleza kuwa lugha ya kifasihi ni lugha ambayo hutumiwa kwa njia ya kisanaa yanahusisha matumizi ya lugha ambayo si ya kawaida.

Hivyo basi, lugha ya kifasihi ni ule ubunifu unaotumiwa na mtunzi wa kazi ya fasihi ili kufikisha ujumbe kwa jamii iliyokusudiwa.

Ni kweli kwamba hakuna lugha ya kifasihi bali kuna matumizi ya lugha katika fasihi kwani rai hii imeshadadiwa na wataalamu mbalimbali kama Njogu na Chimera (2011:8-9) wanashadadia rai hii kuwa hakuna lugha ya kifasihi bali lugha ya lugha ya kifasihi huigeuza lugha ya kawaida kuwa lugha ya kifasihi, hii ina maana kwamba kauli isemwayo kuwa kuna lugha ya kifasihi iliyoteula, inapwaya. Lugha zote hutumia sitiari, jazanda, methali n.k. Hivyo basi,  tutafute kitu kingine cha kueleza dhana ya fasihi mbali na matumizi ya lugha.

Hivyo basi, tunathibitisha rai hii kwa kutumia mawazo ya Wamitila (2008:67-107) kama ifuatavyo:

Lugha na suala la uteuzi

Wamitila (2008:69) uteuzi wa maneno katika kazi ya fasihi hutegemea malengo ya kimawasiliano na kisanii ya mtunzi, japo kuwa ushairi huchukuliwa kama tokeo la matumizi ya lugha kwa njia maalumu hata hivyo haina maana kuwa uteuzi wa namna hii haupatikani katika nathari hivyo basi, ikiwa tuna lugha ya fasihi tunatarajia lugha hiyohiyo itumike katika kazi za kifasihi kama riwaya, tamthiliya na ushairi lakini sivyo tunavyotarajia kwani ushairi una namna ya uteuzi wake maalumu ambao ni tofauti na nathari zingine. Mfano ushairi una mtindo wa udondoshaji wa maneno lakini kazi nyingine kama riwaya zikitumia mtindo huo huonekana kama ni njia hasi ya kujibainisha.

Lugha na suala la lahaja na lafudhi;

Lahaja ni lugha ambayo ina sifa za kiisimu zinazoitenga na vilugha vingine katika lugha fulani maalumu. Msingi wa kuwepo kwa lahaja tofauti na wa kijiografia, uchumi na misingi mingine katika jamii inayohusika. Lafudhi ni dhana inayorejelea sifa za kimatamshi katika matumizi ya lugha ambazo zinahusisha na mtumiaji maalumu wa lugha. Lugha ya Kiswahili ina lahaja nyingi za kijiografia kama vile Kimvita, Kipemba, Kimtang’ata n.k. Uchunguzi wa fasihi ya Kiswahili unadhihirisha tofauti hizi katika matumizi ya lugha ya kazi za waandishi kadha. Toafauti za lugha huweza kutokeza katika kiwango cha lafudhi ya mzungumzaji maalumu anayehusika tofauti hizi zinatokana na ukweli kwamba hakuna wazungumzaji wawili wa lugha wanaotumia au kuzungumza kwa namna sawa kila binadamu ana sifa za kipekee za kiisimu na upekee wa kimtindo ambao unamtambulisha. Sifa hizi zinajitokeza pia katika kazi za kifasihi kwa kuchunguza kwa makini lugha wanazopewa wahusika wenyewe kwa mfano katika kazi za S. A. Mohamedi, (Kiza katika Nuru, 31)

“Haya lete Besa yangu ya jamaa zima…..alianza Ashura. He, Ashura naye kwa rakadha, hata sijatua ukumbini…..”

Naye J. Habwe, (Cheche za Moto, 27)

“Bw. Mulee, iko mambo gani sikia?”

“Mambo yapi? Mulee alimuuliza huku amemlenga macho”

Lugha na Tanzu za Fasihi

Lugha inayotumiwa katika kazi za kifasihi huweza kuwa tofauti kutegemeana na utanzu wa fasihi unaohusika. Ipo miundo ya lugha ambayo inahusishwa zaidi na utanzu mmoja wa fasihi kuliko tanzu nyinginezo kwa mfano utanzu wa ushairi unatumia msamiati wa kale ukilinganishwa na utanzu wa riwaya na tamthiliya. Pili, utanzu huu wa ushairi umetumia msamiati maalumu ambao unapatikana tu katika utanzu huo pia kama tunavyoona inawezekana kazi za kifasihi zikayakiuka matarajio haya ya matumizi ya lugha na kuchanganya lugha tofauti tofauti.

Lugha na Usimulizi.

Usimulizi wowote wa kazi za kifasihi hutegemea lugha kwa kiasi kikubwa, lugha ndio nyenzo kuu ya sanaa ya fasihi. Kwa misingi hiyo ubunifu na usimulizi ndio unaleta utofauti kila msimulizi ndio hutumia ubunifu wake tofauti na wasimulizi wengine ili kuvutia hadhira yake

Lugha na Sajili.

Lugha hutofautiana kutegemeana na mazingira/muktadha inakotumiwa huu ndio msingi wa kile kinachojulikana kama rejesta. Rejesta hizi huwa na sifa kadha wa kadha ikiwemo uwanja au mandhari, lengo la mahusiano n.k. Hakuna namna moja ya uwasilishaji wa kazi moja huweza kutofautiana kutokana na dhamira, wahusika na tamathali za semi. Hivyo, lugha ni nyenzo kuu ya kukuza na kuendeleza maudhui na sajili kama kipengele muhimu cha lugha hiyo ambacho kinashirikiana katika kuvyanza dhamira ya kazi inayohusika na sajili inayotawala. Katika kazi fulani huashiriwa na kuelekezwa na uteuzi wa msamiati, tamathali za semi na motifu zinazoelekezwa. Vilevile, suala la sajali na usawiri wa wahusika hutegemeana na matumizi ya lugha katika muktadha maalumu hutambulisha sajili inayohusishwa na wahusika wanaopatikana katika mazingira fulani kama ni wasomi, wakulima au wafugaji. Pia, sajili na uashiriaji na tamathali za semi hapa tunaangalia mbinu za uashiriaji zinazotumiwa na mtunzi pamoja na tamathali za semi zinazoteuliwa lazima pawepo na mwingiliano wa muktadha na mazingira yanayohusika au sijali inayotumia mbinu za uashiriaji na tamathali za usemi ni mbinu zinazotumiwa na msanii au mwandishi na zinapaswa kutumiwa kwa njia ya kuendeleza hilo.

Utata na Usayakini wa lugha na maana katika fasihi.

Utata ni sifa ya kilugha, kiusemaji ambayo huweza kuwa msingi wa kueleweka kwa neno, kirai au kauli kwa namna tofauti. Hata hivyo,  utata si tamathali au mbinu za kifasihi ambayo huteuliwa na mtumiaji bali ni sifa ya kiuasilia ambayo hufungamana na lugha yenyewe. Utata wa kifasihi huweza kutokea kutegemea sauti, maana au miundo. Hivyo basi, utata wa kifasihi unatokana na matumizi ya tamathali za semi kama tashbiha, sitiari na taashira. Utata haupatikani tu katika matini za kazi za kifasihi bali hata katika mazungumzo ya lugha ya kila siku.

Lugha na suala la uteuzi,

Uteuzi wa lugha katika kazi ya fasihi unaofanywa na mtunzi wa kazi husika na uteuzi huu unathibitiwa kwa kiasi kikubwa na malengo ya kimasiliano ya kisanii ya mtunzi maalumu. Suala hili la uteuzi wa lugha hujitokeza kwa uwazi katika ushairi, ushairi huchukuliwa kama tokeo la lugha kwa njia maalumu hii aina maana haupatikani katika nathari zingine vilevile zipo riwaya nyingi zinaakisi mtindo wa lugha inayohusishwa na ushairi kama vile mtindo wa lugha inayohusishwa na ushairi kama vile mtindo wa udondoshaji. Sifa hii pia inapatikana katika kazi za Shaaban Robert, S. A. Mohamedi.

Hivyo basi, kimsingi hakuna lugha ya fasihi bali kuna matumizi ya lugha katika fasihi kwa mfano ukichunguza kwa undani zaidi tutaona hakuna lugha au mtindo mmoja ambao unapatikana katika kazi zote za kifasihi. Kila mtunzi ana namna yake ya ubunifu katika uandishi na usimulizi wa kazi za kifasihi na sio namna moja ya kujibainisha.

MAREJELEO

Habwe, J. na Karanja, P. (2012) Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers Ltd.

M’ngaruthi (2015) Fasihi Simulizi na Utamaduni. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Mulokozi, M. M. (2017) Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili, Kazi za Fasihi Vyuoni na Vyuo Vikuu. Dar es Salaam: Moccony Printing Press.

Njogu, K na Chimerah, R. (2011) Ufundishaji wa Fasihi; Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Njogu, K na Wafula, R. M. (2013) Nadharia za Uhakiki wa Fasihi. Nairobi: The Jomo Kenyatta Foundation.

Wamitila, K. W. (2008) Kanzi ya Fasihi Misingi ya Uchanganuzi wa Fasihi. Nairobi: Vide~Muwa Publishers.

_____________ (2016) Kamusi Pevu ya Kiswahili. Nairobi: Vide~Muwa Publishers.

Post a Comment

0 Comments