Header Ads Widget

Responsive Advertisement

Kwa kutumia mifano dhahiri eleza mikondo mbalimbali ya Riwaya ya Kiswahili.





Swali hili limegawanyika katika sehemu tatu, ambazo ni utangulizi, kiini na hitimisho. Katika utangulizi ufafanuzi wa dhana ya riwaya pamoja na historia fupi ya Riwaya ya Kiswahili imetolewa, katika kiini kuna ufafanuzi wa mikondo ya riwaya ya Kiswahili na mwisho ni hitimisho la swali.

1.0 Utangulizi

1.1 Fasili Mbalimbali

Msokile (1992), riwaya ni kazi ya sanaa ya kubuni, ni maandishi ya nathari yanayosimulia hadithi ambayo kwa kawaida ina uzito, upana, urefu wa kutosha, ina wahusika mbalimbali wenye tabia za aina nyingi; ina migogoro mingi mikubwa na midogo. Fasili hii imetolewa kwa kuzingatia sifa za riwaya.

Mulokozi (1996) wanaeleza kuwa, riwaya ya Kiswahili ni masimulizi marefu yakinathari yaliyochangamana kiasi, yenye kuzungumzia tajriba ya maisha ya binadamu kwa ubunifu. Fasili hii imejikita katika kigezo cha urefu, lakini haielezi urefu huo unapaswa kuwa kiasi gani.

Kwa ujumla riwaya ni masimulizi ya kubuni ya kinathari yenye msuko au mpangilio fulani wa matukio au ploti inayofungamana na wakati au kusawili wakati na yenye visa vingi vivavyotendeka katika wakati fulani na yenye mawanda mapana yenye mchangamano wa dhamira, visa na wahusika.

1.2 Historia ya Riwaya ya Kiswahili Tanzania

Utanzu wa riwaya umechelewa sana si Tanzania tu bali katika Afrika na nchi zinazoendelea karibu zote. Nathari bunifu simulizi kama vile hekaya na ngano iliyosimuliwa kwa mdomo ndizo zilitawala miongoni mwa jamii. Kwa upande wa fasihi andishi maandiko ya kishairi hususani tendi za Kiswahili katika hati za Kiarabu ndizo zilizotawala katika upwa wa Afrika mashariki. Wazungu walipofika maeneo haya ya Afrika mashaiki wakiwa na teknolojia yao mpya ya uandishi bado kulikuwa na utengano katiyao  na waarabu hivyo pakawa na majilio ya taratibu ya maandiko ya kinathari. Nathari ya kwanza kuandikwa ilikuwa ni  ya Sheikh Ali bin Hamed ya Habari za Mrima (1880) na kuchapishwa rasmi (1935) vilevile Habari za Wakilindi ya mwaka (1895).

Kipindi cha waingereza kuliibuka kazi nyingi za nathari za kibunifu ambazo kutokana na elimu ya waingereza walielekeza juhudi za kupata kwa kuandia na kutafsiri ndiyo maana kuna tafsiri nyingi wakati huo mfano. Hadithi za Esopo, Safari ya Msafiri, Kisiwa chenye Hazina, Safari ya Gulliver. Kisiwa Chenye Hazina na vingine vingi. Waandishi wengine walianza kuandika kazi zao kwa mfuatano wa kimkondo. Mikondo hiyo imeelezwa kama ifuatavyo:

2.0 Kiini cha Swali

2.1 Mkondo wa kisafari na kimaadili.

Mkondo huu unajumuisha riwaya za mwanzo kabisa za Kiswahili, zilizokuwa zikihusisha safari na maadili. Kazi ya kibunifu ya kwanza ilikuwa ni Uhuru wa Watumwa (1934) iliyoandikwa na James Mbotela kisha zikafuatiwa na riwaya za Shaban Robert ambazo ni kusadikika (1951), Kufikirika (1952) na Adili na Nduguze (1952). Kazi hizi zilihusu kufundisha maadili na mwenendo mwema katika maisha. Maranyingi riwaya hizi huchukua muundo wa kisafari, vilevile muundo huwa katika kaida fulani za kifasihi ambazo ni mwendelezo wa mazungumzo au dayalojia, matumizi ya muda au wakati sifa za kiujumla na utumizi wa mubalagha.

2.2 Mkondo wa Kiethografia

Mkondo huu pia unaweza kuitwa mkondo wa kinyaraka, hii ni kutokana na sifa yake kubwa ya kuhifadhi maswala muhimu ya kijamii na kiutamaduni. mathalani, mila na desturi na historia ya jamii. Mifano ya riwaya zinazopatikana katika mkondo huu ni riwaya ya Bwana Myombokere na Bibi Bugonoka iliyoandikwa na Anicenti Kitereza (1945) na kuchapishwa baadaye (1981). Riwaya hii imesimulia historia na tamaduni za Wakerewe ikiwemo mila na desturi na maisha yao kiujumla pamoja na kipindi cha ujio wa wageni. Vilevile riwaya ya Kurwa na Dotto (1951) iliyoandikwa na Salehe Farsy, riwaya hii inasawiri mila na destiri za watu wa unguja pia mwaka (1971) riwaya nyingine za kiethnografia iliyoibuka ni Mzishi wa Baba Anaradhi iliyoandikwa na Felician Nkwera ambayo ilielezea maisha ya wapangwa ambao ni watu wa mwambao wa ziwa nyasa.

2.3 Mkondo wa Kihalifu au Kipelelezi

Mkondo huu wa uhalifu au kipelelezi ulijitokeza katika fasihi ya Kiswahili mwishoni mwa muongo wa 50 wa karne ya ishirini. Riwaya ya kwanza kuibuka katika mkondo huu ni riwaya ya Mzimu wa Watu Wakale (1957- 1958) iliyoandikwa na Mohamed Said Abdulla. Riwaya hii ilikuwa ni matokeo ya mashindano ya uandishi wa hadithi za kubuni kwa lugha ya Kiswahili kama ilivyoandaliwa na kamati ya lugha ya Kiswahili Afrika Mashariki. baadaye miaka ya 60 Faraji Katalambulla alienda riwaya katika mkondo huu iliyoitwa Simu ya Kifo (1966). Mwandishi M.S. Abdulla alifanikiwa kupata mfuasi mzuri mwishoni mwa miaka ya sabini ambaye ni Elistabulus Musiba aliandika hadithi zake za kiualifu, kipelelezi na kimapenzi. Musiba aliandika riwaya ya kikosi cha kisasi (1979) akiwa na muelekeo uleule wa Abdulla.

2.4 Mkondo wa kijamaa (kinostalgia na kiprognosia)

Mkondo huu katika riwaya ya Kiswahili umetokana na mabadiliko ya hali ya kisiasa nchini Tanzania kupitia Azimio la Arusha la mwaka (1967), hivyo hali hiyo iliathiri vikubwa muktadha wa Fasihi ya Kiswahili, ushairi na tamthiliya ni tanzu za mwanzo katika kusawiri mabadiliko hayo. Lakini riwaya ilichelewa kuyapokea mabadiliko hayo, kazi za fasihi zilisawiri mabadiliko hayo kwa namna mbili tofauti kwani kuna waandishi waliona ujamaa katika jicho la namna wahenga wetu walivyoishi pamoja na hivyo na jamiii yetu irejee kulenyuma, pia kuna waandishi walioona kuwa matarajio kwamba kuna ujenzi wa jamii mpya itakayoishi vyema kuliko hii ya sasa, kundi hili liliandika kwa kusawiri ndoto zao kwa wakati ujao. Riwaya ya kwanza katika mkondo huu ilikuwa ni ya "Njozi ya Usiku" (1972) iliyoandikwa na W. Seme ambayo nayo inashadadia maisha ya wahenga kwa kusisitiza ushirikiano. Mifano za Kiprognosia ni kama vile Ndoto ya Ndaria (1975) iliyoandikwa na J. Ngomoi.

2.5 Mkondo wa Uhalisia – Teti (wakihakiki)

Mkondo huu wa uhalisia ulijitokeza mwishoni mwa miaka ya (1970 - 1980). Katika kipindi hiki hali ya uchumi ilianza kudidimia. Hali hii ya kudidimia kwa uchumi ilisababisha kuibuka kwa kazi za kinathari ambazo zilielekeza kidole cha mashtaka kwa viongozi wa serikali kwa uroho wao, usaliti na rushwa, viongozi ambao hawakutaka kuwasaidia viongozi wadogo ambao bado walikuwa na imani katika ujenzi wa jamii mpya. Mifano ya riwaya hizo ni Nyota ya Huzuni (1978) iliyoandikwa na Liwenga na Njozi Iliyopotea (1979) ya Mung'ong'o pia riwaya zingine ni kama Kichwa Maji (1974) na Gamba la Nyoka (1975) zilizoandikwa na Kezilahabi, Kabwela (1978) na Harusi (1984) za Abdallah. J. Safari



2.6 Mkondo wa Kitafakuri ( mkondo wa kimajaribio)

Mkondo huu uliibuka miaka ya (1970-1980) ambapo wasomi walituliza vichwa vyao na kuanza kutumia maarifa yao kueleza na kuchambua maisha ya kijamii. Miongoni mwa waandishi walioibuka katika mkondo huu ni Euphrase Kazilahabi aloyeandika Rosa Mistika (1971) kama nathari bunilizi iliyoeleza kwa uwazi ukweli wa maisha na baadaye na wanamaadili wa kimagharibi kwa kukiuka maadili ya kijamii. Pia aliandika baadaye kazi nyingine za kidhanaishi mfano wa kazi hizo ni kama Dunia Uwanja wa Fujo (1976), Nagona (1987) na Mzingile (1990). Baada ya kazi hizo waandishi wengine waliathiriwa na mtindo wa kezilahabi na kuanza kuandika kazi zao kwa mtindo huo ni kama; Willium Mkufya na kazi yake ya Ziraili na Zirani, Said Ahmed Mohamed na bunilizi la  Babu Alipokufa (2001). Hivyo mkondo huu umeingiza namna mpya ya uandishi katika nathari bunilizi.

2.7   Mkondo wa ufungwa.

Mkondo huu ni mgeni katika nathari bunulizi za kiswahili. Haya ni maandiko ambayo yanaweza kuwa ni ya kitawasifu au kiwasifu yakisawiri matukio ya gerezani au magereza. Maandiko haya yamekuweko katika nchi nyingine kama vile nathari ya Nelson Mandela, long walk to freedom (1995) aliyoiandika kuhusu maisha yake ya ufungwa huko Afrika ya kusini. Kenya mwandishi wa nathari ya ufungwa ni ya Ngugi wa Thiong'o ambaye yameathiriwa sana na kufungwa  kwake kutokana na harakati zake za kuushambulia ubepari unaoletwa na ukoloni mamboleo. Baadhi ya vitabu vyake vimmetafsiriwa katika kiswahili kwa mfano Ntaoa Nikipenda na Shetani Msalabani. Nigeria yuko Wole Soyinka na Malawi yupo Jack Mapanje na katika Tanzania mwandishi wa nathari ya ufungwa hadi hivi sasa ni Maulid Haji aliyejitokeza katika miaka ya 90 na kuandika Umleavyo (1990) hadithi ambayo inasawiri maisha ya rumande na msimulizi wa kazi hiyo akiwa yeye mwenyewe.

3.0 Hitimisho

Kwa kuhitimisha. Mikondo ya riwaya ya  Kiswahili inaweza kugawanyika katika vipindi tofauti tofauti vya miaka. Kwani katika kipindi fulani cha miaka kuna uwezekano wa kuibuka kwa  mikondo mbalimbali ya riwaya ya Kiswahili inayojitokeza. Mathalani (1960 -1970) kulikuwa na mkondo wa uhalisia, mkondo wa kijamaa, mkondo wa kitafakuri na mkondo wa kijamaa.

                                                      MAREJELEO

Madumulla, J. S (2009) Riwaya ya Kiswahili: Nadharia, Historia na Misingi ya Uchambuzi.

                                         Mture Educational Publishers Limited; Dar es Salaam

Msokile, M.(1992) Misingi ya Hadithi Fupi. Dar es Salaam Universty Press:

                                         Dar es Salaam

Mulokozi, M. M. (1996), Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili; Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili,

                                             Dar es salaam.









                          













































 













Post a Comment

0 Comments