Header Ads Widget

Responsive Advertisement

changamoto katika kuhakiki fasihi ya kiswahili kihistoria

 

CHANGAMOTO ZILIZOMO KATIKA KUHAKIKI FASIHI YA KISWAHILI KIHISTORIA KWA KUREJELEA TAMTHILIA YA MASHETANI.

Ebrahim Hussein alizaliwa mnamo mwaka wa 1943. Aliandika tamthilia yake ya kwanza,Kinjeketile (1969), Jogoo Kijijini (1976), Mashetani (1971) na Arusi (1980). Tamthilia ya Mashetani iliandikwa 1971 takriban miaka kumi baada ya Tanzania kujinyakulia uhuru. Harakati za waafrika kupigania uhuru, maono na azma yao ya utawala bora wa Mwafrika ndio yalimchochea mwandishi huyu kuandika tamthilia hii.

Nchi ya Tanganyika ilipata uhuru tarehe 1/5/1961 ikiongozwa na Mwalimu Julius Nyerere, na
kisha kuungana na serikali ya Zanzibar na kuwa Tanzania mwaka wa 1964 chini ya uongozi wa
Abeid Amaan Karume.Waafrika waliokuwa na elimu ya juu wakachukua nyadhifa mbalimbali za
uongozi. Kinyume na matarajio ya wananchi wa kawaida, viongozi hawa wakawa ‘Wazungu
Weusi'. Hii inamaanisha kuwa walichukua mienendo yote na kasumba zote za wakoloni. Visa
vya ufisadi, ukabila, ubinafsi na tamaa ya kujilimbikizia mali ikawa hali ya kawaida.

Isitoshe, serikali ya Zanzibar iliamua kutaifisha mashamba yaliyokuwa yamenyakuliwa na viongozi
waliokuwepo katika enzi za utawala wa wakoloni na kugawia viongozi hawa wapya. Hali hii
ikazua utabaka kwani, jamii ambazo zilikuwa tajiri hapo awali zikaanza kutamba katika
mazingira ya uchochole. Waliokuwa maskini awali lakini wenye kisomo cha kimagharibi
wakaanza kupanda ngazi ya ufanisi kiuchumi kwa haraka zaidi kama wasemavyo, "kulala
maskini na kuamka tajiri".

Haya ndio mazingira aliyokulia ndani mwandishi Ebrahim Hussein. Rais Nyerere alipotanabahi udhaifu huu katika serikali yake, akaamua kubuni sera mpya ambayo aliona kuwa ingeondoa utabaka na kuleta usawa wa kiuchumi katika jamii. Akazindua Azmio la Arusha mnamo mwaka wa 1967. Hii ni sera ya serikali iliyonuia kuunda mfumo wa Ujamaa.


Mfumo huu ulikusudia kuondoa pengo la utabaka na kufanya jamii ya Watanzania kuishi kwa undugu. Mwanzoni, mfumo huu ulivuma sana kwa kuinua kiwango cha elimu, afya na kupunguza utabaka. Hii ni kwa sababu alitaifisha sekta zote za uchumi na kuanzisha mfumo wa kilimo kupitia kwa mashamba yaliyokuwa yametaifishwa vijijini. Kiwango cha uzalishaji mali kikaongezeka kufikia hali ya Tanzania kuanza kujitegemea.

Sera hii haikudumu kwa sababu mfumo huu ulianza kukumbwa na changamoto za aina mbalimbali. Kwanza, wawekezaji wa kibinafsi walianza kupungua kwa sababu sekta nyingi za uchumi zilikuwa zimetaifishwa. Bidhaa zilizozalika kuanzia mazao ya mashamabani hadi bidhaa za viwandani zikakosa soko la kimataifa kwa sababu ya mfumko wa bei ulimwenguni. Mfumko huu ukaathiri pia taifa kuu la Tanzania hadi kuifanya serikali kushindwa kutekeleza huduma muhimu.

Watu wengi wakatamaushwa kwa sababu ya matatizo mengi ya kiuchumi. Kina cha matukio haya ya kihistoria ndio yaliyomchochea Ebrahim Hussein kuandika tamthilia ya Mashetani.

CHANGAMOTO ZA KUHAKIKI FASIHI YA KISWAHILI KIHISTORIA.

Kimani na Chimera(1999), wanaeleza kuwa kupitia kwa maigizo katika Mashetani, msomaji,msikilizaji au mtazamaji huanza kufahamu mahusiano kati ya viongozi na waongozwa, uhuru na ukoloni mamboleo, ukoloni mkongwe, na unyanyasaji wa Waafrika na Wakoloni wazungu. Vile vile mtafaruku kati ya mabwana waliokuwa na madaraka mbeleni na wale wanaochukuwa nyadhifa za uongozi baada ya uhuru unaangaziwa. Matukio hayo japo ni ya mwandishi yanaafiki vilivyo historia ya Tanzania. Mulokozi, M.M alidokeza vigezo vinne vikuu vya kuzingatia iwapo utalinganisha fasihi na historia. Navyo ni matukio, wahusika na mbinu au mtindo wa uandishi. Kwanza, matukio jinsi yalivyotukia katika Historia huwa tofauti zaidi kuliko jinsi yanavyotukia katika mawanda ya fasihi. Baadhi ya sehemu za matukio katika hadithi za fasihi zaweza kutokea kama zisizo za kweli, licha ya kuwa hadithi yaweza kuwa ya kuvutia au yenye ubunifu mkubwa.

Matukio katika fasihi hurejelea wahusika wa kihistoria ambao huundwa upya kisanaa. Historia huangazia matukio ya wahusika jinsi wanavyojitokeza katika hali halisia. Historia ya Tanzania iliangazia wahusika halisi waliochangia katika kuchipuka kwa mapinduzi kisiwani Zanzibar kama vile Abedi Karume na Sultani. Wahusika hawa kihistoria walifafanuliwa kihistoria kwa kueleza sifa na tabia zao asilia. Lakini fasihi, inawajenga wahusika wapya wa kubuni kama vile jamii ya Juma na Kitaru, wanaoafiki viongozi hawa.

Katika Historia mkazo huwekwa kwa matukio muhimu ambayo yana mchango mkuu katika mkondo wa matendo yatakayoathiri maisha ya binadamu.Tukio kuu katika Historia ya Tanzania ni mapinduzi ya Sultani wa Zanzibar na kujinyakulia uhuru kwa Waafrika. Kwa upande mwingine, matukio makuu ya historia hutumiwa kama muktadha wa matendo ya hadithi ambayo huweza kuwa ya ukweli au ya kubuni. Katika tamthilia ya Mashetani, tukio la Shetani kumpa Binadamu kisu (uk 8), inaashiria jinsi mzungu alivyopanga na kumpa Mwafrika uhuru kwa hiari yake bila kushinikizwa. Tukio hili huenda likawa si la kweli bali ni ubunifu tu wa mwandishi kwa sababu kuna vikosi vya wapiganaji ambao walimwaga damu kwa ajili ya kujikomboa.

Fasihi husistiza jinsi wahusika wa matukio madogo madogo ambayo huchopeka katika matukio makuu ya kihistoria hujitokeza.Kwa mfano, fasihi yaweza kutoa msisitizo kwa wahusika shujaa ambao labda katika hali halisia hawakuwahi ishi kamwe. Jamii ya Kitaru na Juma ni ya kubuni tu, huenda jamii kama hizi hazikuwahi kuishi kama jirani mjini Dar es salaam kama anavyodai mwandishi.Mwanafunzi ambaye angependa kuelewa zaidi historia ya matukio haya, huenda hatanufaika zaidi akiegemea matukio ya wahusika hawa.

Kwenye fasihi, migogoro ya taifa au jamii hufasiriwa katika hisia na matendo ya watu binafsi. Mgogoro kati ya Juma na Kitaru unaafiki migogoro iliyojitokeza kati ya makabaila na mabwenyenye kihistoria:


Juma: Hatuonani tena.

Kitaru: Kwa nini?

Juma: Sababu nyingi.

Kitaru: Mojawapo?

Juma: Mpanda ngazi na mshuka ngazi hawawezi kushikana mikono. (Uk.55-56)

Katika kifungu hiki taswira ya utabaka inasawiriwa kupitia kwa mtafaruku wa uhusiano uliopo kati ya Juma na Kitaru. Kama ingekuwa historia, ingeangazia sifa halisi za tabaka hizi mbili bila kujikita kwa wahusika wawili tu katika jamii.

Fasihi inayofanikiwa sana ni ile inayojikita zaidi katika migogoro mikali zaidi ya kihistoria. Fasihi ambayo haitaangazia migogoro mikali ya kijamii ya kufa na kupona kama vita, utabaka au mapinduzi hupuuziliwa mbali.Tamthilia ya Mashetani ilivuma na kubobea zaidi kifasihi kuliko tamthilia zingine za wakati huo kwa sababu iliafiki mapinduzi na kuzuka kwa utabaka miongoni mwa Waafrika wenyewe, kinyume cha matarajio. Mwanafasihi ambaye angependa kufurahia kusoma matukio hayo madogo huenda asipate makala ya kutosha.

Historia hueleza ukweli jinsi ulivyotokea. Kwa mfano Azimio la Arusha la mwaka wa 1967, limeelezwa kwa undani zaidi kupitia taaluma ya historia. Mipangilio, sera na mikakati yote ya utekelezaji wake yalielezwa kinagaubaga katika taaluma ya historia.Watendaji wa matukio katika historia hawapewi sifa au tabia kinyume cha jinsi walivyokuwa kihalisia. Lakini baadhi ya matini ya fasihi huwapa wahusika wao majukumu mapya kinyume cha hali ilivyokuwa kihistoria. Katika Mashetani, mwandishi hakuzama zaidi kueleza suluhu la tatizo la mgogoro wa kitabaka kama inavyobainika katika historia kwa kuanzishwa kwa ujamaa.

Wahusika wa Historia ni watu waliopata kuishi. Lakini katika fasihi ni wahusika wa kubuni. Msomaji wa fasihi huona matukio ya kihistoria kupitia kwa wahusika wa matini. Kisa cha Binadamu kumwua Shetani kwa kumdunga kisu katika tamthilia ya Mashetani kinadhihirisha tukio la historia la Tanzania kujinyakulia uhuru mnamo mwaka wa 1964 kutoka kwa Wazungu. Changamoto zinazomkumba msomaji wa makala haya ni kwamba hataweza kusawiri hali halisi ya kihistoria jinsi matukio hayo yalitukia. Kabla ya kuuawa, Shetani anapendekeza kusherehekea kifo chake, kisha anakubali kumpa binadamu kisu ili amuue. Kila pigo la kisu kwa shetani linazua kicheko.

Baada ya mauaji Binadamu anashindwa kujitambua kama kweli alimuua Shetani au la. Kadhia hii ilinuia kumfahamisha msomaji namna na jinsi Mwafrika alivyonyakua mamlaka kutoka kwa mkoloni.Kwamba mzungu aliamua tu kumpa uhuru kwa hiari yake bila kushinikizwa, na baadaye athari za kuendelea kuwepo kwa ukoloni mamboleo ukaendelea kudhihirika kupitia kwa kicheko. Kimsingi ni kuwa fasihi hueleza matukio yake kwa ubunifu mkubwa kuliko huistoria. Ubunifu huu huenda ukamshinda msomaji wa kawaida kuelewa namna matukio hayo yalivyotukia kihistoria. Ni kweli kihistoria kuwa wapiganiaji uhuru walikufa na wengine kujeruhiwa, kinyume na inavyosawiriwa tamthilia kuwa Waafrika walipewa uhuru moja kwa moja kwa njia ya mzaha.

Tabia za wahusika wa fasihi wakati mwingine hupewa sifa za chuku. Mhusika Shetani ana uwezo wa kurukia kwenye tawi, aweza kuamua kuuawa na namna ya kuuawa kwake. Vile vile, anapodungwa kisu haonyeshi huzuni wala kilio bali anaonyesha furaha kupitia kicheko. Wahusika wa historia wanadhihirisha tabia zao asilia. Historia inapozungumzia mapinduzi ya Abedi Karume ya Zanzibar, husimulia tabia halisi ya wanaharakati wa mapinduzi. Jambo hili huwanyima wanafasihi uhondo wa kuelewa sifa halisi za wahusika wao.

Wahusika wa Historia ni watu waliopata kuishi. Lakini katika fasihi ni wahusika wa kubuni. Msomaji wa fasihi huona matukio ya kihistoria kupitia kwa wahusika wa matini. Kisa cha Binadamu kumwua Shetani kwa kumdunga kisu katika tamthilia ya Mashetani kinadhihirisha tukio la historia la Tanzania kujinyakulia uhuru mnamo mwaka wa 1964 kutoka kwa Wazungu. Changamoto zinazomkumba msomaji wa makala haya ni kwamba hataweza kusawiri hali halisi ya kihistoria jinsi matukio hayo yalitukia. Kabla ya kuuawa, Shetani anapendekeza kusherehekea kifo chake, kisha anakubali kumpa binadamu kisu ili amuue. Kila pigo la kisu kwa shetani linazua kicheko. Baada ya mauaji Binadamu anashindwa kujitambua kama kweli alimuua Shetani au la. Kadhia hii ilinuia kumfahamisha msomaji namna na jinsi Mwafrika alivyonyakua mamlaka kutoka kwa mkoloni.Kwamba mzungu aliamua tu kumpa uhuru kwa hiari yake bila kushinikizwa, na baadaye athari za kuendelea kuwepo kwa ukoloni mamboleo ukaendelea kudhihirika kupitia kwa kicheko. Kimsingi ni kuwa fasihi hueleza matukio yake kwa ubunifu mkubwa kuliko huistoria. Ubunifu huu huenda ukamshinda msomaji wa kawaida kuelewa namna matukio hayo yalivyotukia kihistoria. Ni kweli kihistoria kuwa wapiganiaji uhuru walikufa na wengine kujeruhiwa, kinyume na inavyosawiriwa tamthilia kuwa Waafrika walipewa uhuru moja kwa moja kwa njia ya mzaha. Tabia za wahusika wa fasihi wakati mwingine hupewa sifa za chuku. Mhusika Shetani ana uwezo wa kurukia kwenye tawi, aweza kuamua kuuawa na namna ya kuuawa kwake. Vile vile, anapodungwa kisu haonyeshi huzuni wala kilio bali anaonyesha furaha kupitia kicheko. Wahusika wa historia wanadhihirisha tabia zao asilia. Historia inapozungumzia mapinduzi ya Abedi Karume ya Zanzibar, husimulia tabia halisi ya wanaharakati wa mapinduzi. Jambo hili huwanyima wanafasihi uhondo wa kuelewa sifa halisi za wahusika wao.

 

Mtindo wa lugha ni kigezo kingine ambacho huzua changamoto katika kuhakiki kazi ya fasihi kihisoria. Mbinu za lugha, mbinu za uandishi na mitindo aliyotumia msanii wa fasihi huzua changamoto kwa wanahistoria.Historia hueleza matukio yake kwa njia wazi na yenye muala kiusababishaji. Aidha, tukio la kwanza kihistoria huwa mwanzoni kutokea na la mwisho huwa mwisho. Mwandishi wa fasihi huvuruga kanuni hii kwa kutumia vipengele kama mbinu rejeshi au msuko usio muala. Katika Tamthilia ya Mashetani tukio la Baba Kitaru kurudi nyumbani akiwa na furaha tele linaenda sambamba na lile la Juma kuwa kwao nyumbani kwa kibanda akizungumza na Bibi. Matukio haya yakiwekwa katika muktadha wa mtiririko wa kihistoria huzua changamoto tele. Kwa mfano, katika historia huwezi kuzungumzia athari za vita kabla ya kuangaza chanzo chake. Lugha ya Historia huwa rahisi na wazi ilhali lugha ya fasihi huwa changamano na yenye mafumbo mengi.

Matumizi ya jazanda na taswira humtatiza mwanahistoria anayechanganua matini ya fasihi. Kimani na Chimera (1999), wanatoa mifano ya taswira iliyotumiwa na mwandishi kusawiri matukio mengine tofauti. Shetani awakilisha mkoloni, Binadamu ni Mwafrika mtawaliwa, chewa ni mfumo wa kibepari na ndoto ya Kitaru ni ufunuo wa migogoro ya kitabaka iliyozuka baada ya kutaifisha mashamba. Kadhalika, joka la vichwa saba linaashiria nchi saba za kibepari, manyoya aliyomea Kitaru yanaashiria utajiri au mali.Haitawezekana maudhui kama vile: mahali pa utamaduni halisi wa kiafrika, athari za ukoloni mkongwe, ubwanyenye,na ukoloni mamboleo kueleweka ipasavyo ikiwa mwanahistoria hataainisha na kuelewa lugha hii ya taswira, jazanda na ishara.

HITIMISHO

Jinsi ilivyojadiliwa katika makala hii, ni ukweli usiopingika kuwa kuna uhusiano mkubwa zaidi kati ya fasihi na historia. Lakini kufasiri vilivyo kazi ya fasihi kwa kuegemea taaluma ya historia huzua changamoto nyingi katika ugunduzi na uelewekaji wa matini ya fasihi. Kwa hivyo, ili mwanahistoria aweze kufurahia uhondo wa fasihi, lazima awe makini kuelewa na kubainisha mbinu za kafasihi. Kutokuwa na maarifa na ujuzi wa kiuchanganuzi wa fasihi, kutamfanya mwanahistoria kushindwa kuelewa vilivyo sanaa ya fasihi.

Marejeleo.

Kimani N. Na Chimera, R. (1999).Ufundishaji wa fasihi, nadharia na mbinu.Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.

Rajmund Ohly, (2005). Historical Approach to Swahili Literature.An Open Question.

Kiswahili Juzuu la 68. Dar es Salaam:TUKI

Wafula R. M. na Kimani, M (2007). Nadharia za uhakiki wa Fasihi.Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.
Hussein Ebrahim, (1971).
Mashetani. Nairobi: O.U.P.

 

Post a Comment

0 Comments